0
KULIZUKA vurumai katika shule ya msingi mwanamume alipomiminiwa risasi na kuuawa papo hapo kwa kujaribu kumshambulia Mbunge wa Ndia Stephen Ngare.
Wakati wa kisa hicho cha kushangaza, mlinzi wa mbunge huyo,Bw Joseph Mushumba, na mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi ya Ndando, Bw Sammy Mwangi, walijeruhiwa vibaya.
Bw Ngare alikuwa ametembelea sehemu hiyo kukagua miradi ya maendeleo.
Waathiriwa hao walikatakatwa mara kadha kwa upanga na mvamiaji huyo huku wakimkinga Mbunge huyo ambaye alikuwa analengwa.
Walioandamana na Mbunge huyo, wanafunzi na wazazi walitorokea usalama wao huku milio ya risasi ikitamba hewani.
Pia waliotorokea usalama wao ni maafisa wawili wa polisi waliovalia sare rasmi lakini hawakuwa na silaha zozote. Jukumu la kumkinga Mbunge huyo liliachiwa mwalimu huyo mkuu pamoja na mlinzi wake.
Fujo hilo zilivuruga shughuli za masomo shuleni humo mchana kutwa.
Mbunge huyo alianza ziara yake majira ya saa nne asubuhi akiandamana na maafisa wa Hazina ya Ustawi wa Maeneo Bunge (CDF).
Baada ya kuwasili Ngando, alilakiwa kwa shangwe na wazazi, walimu na wazazi. Alipokuwa akielekea katika madarasa mapya yaliyofadhiliwa na hazina hiyo, mwanamume mmoja alichomoka kutoka kwa umati na kumkabili mbunge huyo.
Alimlenga mbunge huyo tayari kumkata kwa upanga huo lakini mwalimu mkuu akamzuia. Bw Mwangi alijikakamua kumsitiri mbunge huyo lakini akazidiwa nguvu na mvamizi huyo anayetoka lokesheni ndogo ya Thigirichi.
Ni wakati huo ambapo alimkatakata Bw Mwangi mara kadha kichwani kabla ya kumwangusha chini. Ni wakati huo ambapo mlinzi wake alijaribu kumkabili mwanamume huyo lakini naye akakatwa kwenye mkono wake wa kushoto.
Huku akibubujikwa damu, mlinzi huyo alichomoa bastola yake na kummiminia mtu huyo risasi, hali iliyowafanya wakazi hao kutoroka kwa hofu.
Mhasiriwa huyo alianguka chini huku Mbunge huyo na mlinzi wake wakiingia kwenye gari lake na kufululiza hadi kituo cha polisi cha Sagana.
Baadaye, waathiriwa walipelekwa katika kituo cha afya cha Saganga kisha wakahamishwa hadi hospitali ya Jamii mjini Karatina baada ya hali yao kudhoofika.
Mwalimu huyo mkuu alijeruhiwa mara kadha na akapelekwa hospitalini akiwa amezimia.
Mshtuko
Haikubainika mara moja ni kwa nini mvamizi huyo alitaka kumdhuru Mbunge lakini wafuasi wake walishuku alichochewa kisiasa.
Bw Ngare ambaye alionekana kuwa na mshtuko mkuu akikataa kuzungumzia jaribio hilo la kutaka kumuua. “Bado nimeshtuka na siwezi kusema chochote wakati huu,” alisema katika kituo cha polisi alipoenda kuandikisha taarifa.
Bw Ngare aliahidi kutoa taarifa ya kina baada ya kuhimili mshtuko huo akisema hicho ni kisa cha kushtua.
“Hiki ni kisa cha kushangaza na nitahitajika kuwa katika hali shwari kabla ya kutoa taarifa yoyote,” aliongeza huku akifarijiwa na naibu Kamishna wa Kaunti ya Kirinyaga Bi Roda Onyancha.
Kasisi wa kanisa la Anglikana Samuel Kanjobe ambaye ni mwanachama wa kamati ya CDF alilaani uvamizi huo.
Mkazi wa sehemu hiyo  Bw Maina Kamonde alisema mwanaume huyo alikuwa ameficha panga ndani ya shati lake kisha akachomoka mbele alipomwona Mbunge huyo. 
Bw Kamonde aliwakosoa maafisa wa usalama kwa kuzembea kazini. “ Askari wa Utawala walifahamu kwamba mbunge alikuwa anakagua miradi ya maendeleo shuleni humo lakini hawakutilia maanani suala hilo, ndio maana wakatoroka kwa waliposikia milio ya risasi kwa kuwa hakubeba bunduki,” alisema. 
Gavana wa kaunti hiyo Joseph Ndathi alilaani kisa hicho na kuwataka polisi kufanya uchunguzi wa kina.

Post a Comment

toa maoni yako hapa pia usisahau kuweka coment

 
Top

SOMA HABARI KEM KEM KUPITIA BLOG YAKO PENDWA YA HISIA ZA MWANANCHI HAPA

X