![]() |
Gazeti la News of Rwanda ambalo linatajwa kuwa mshirika mkubwa wa Serikali ya nchi hiyo, katika toleo lake la Jumapili iliyopita, liliandika kuwa Rais Kikwete amekutana na waanzilishi wa chama cha upinzani nchini humo cha Rwanda National Congress (RNC) na makamanda waandamizi wa waasi wa FDLR.
Habari iliyoandikwa na gazeti hilo, imebainisha kuwa kikao hicho cha Rais Kikwete na watu hao kilifanyika kwenye makazi binafsi ya Rais Kikwete.
![]() |
Wameandika kuwa viongozi wa RNC waliokutana na Rais Kikwete ni Mratibu wa chama hicho, Dk. Theogene Rudasingwa na mshauri wake, Condo Gervais.
Katika kikao hicho, News of Rwanda lilidai kuwa kundi la waasi wa FDLR, liliwakilishwa na Katibu Mtendaji wake, Luteni Kanali Wilson Irategeka na Kanali Hamadi ambaye ni kamanda wa operesheni.
Luteni Kanali Irategeka kwa sasa anatajwa kuwa ndiye nembo ya waasi wa Rwanda wa kundi la FDLR na mara kwa mara amekuwa akionekana kwenye mahojiano na vyombo vya habari.
News of Rwanda liliendelea kuandika kuwa, majina hayo anayotumia Luteni Kanali Irategeka si yake na kwamba jina lake kamili ni Ndagijimana.
Viongozi hao wa FDLR wote wanaishi Washington, nchini Marekani na kwamba wanasafiri kwa kutumia hati za kusafiria za Tanzania.
Hata hivyo, News of Rwanda wameshindwa kuthibitisha madai yao ya pasi za kusafiria za waasi hao kama zimetolewa na Serikali ya Tanzania, au zilipatikana kwa mlango wa nyuma.
Aidha gazeti hili lilikwenda mbali zaidi kwa kudai kuwa Januari 19, mwaka huu, Waziri Mkuu wa zamani wa nchi hiyo, Faustin Twagiramungu alikuwa Tanzania kwa shughuli kama iliyofanywa na waasi wa FDLR.
Walidai kuwa hata hivyo aliondoka Tanzania Alhamisi ya wiki iliyopita, kuelekea Lyon, nchini Ufaransa ambako alikuwa aongoze kikao cha kundi lake la kisiasa la RDI na Rwanda RWIZA.
Limedai, Twagiramungu aliondoka kabla ya timu ya RNC haijawasili Dar es Salaam, ingawa Twagiramungu pia alipaswa kuwa pamoja na RNC na FDLR.
News of Rwanda halikuweza kubainisha kilichopelekea Twagiramungu kuamua kukaa mbali na wenzake hao, ingawa walidai kwamba Waziri Mkuu huyo wa zamani hataki kuingia tena katika ndoa ya kisiasa na kundi linalohusisha waanzilishi wanne wa RNC.
Twagiramungu ndiye Waziri Mkuu wa kwanza kushika wadhifa huo mara baada ya kumalizika kwa mauaji ya kimbari, ambapo alishika wadhifa huo kwa kipindi cha mwaka mmoja na baadaye kujiuzulu.
Limebainisha kuwa, Twagiramungu amekuwa na uhusiano mbovu na Dk. Rudasingwa na Kayumba Nyamwasa kutokana na kuwa sababu ya yeye kushindwa kutekeleza majukumu yake na kuamua kuachia ngazi.
Wawili hao wamedaiwa kuwa walikuwa maofisa waandamizi katika nyadhifa kubwa kisiasa na kijeshi nchini Rwanda.
News of Rwanda limebainisha kuwa, Twagiramungu na makundi mengine ya waasi ya Rwanda, yameapa kutoingia katika ushirika wa kisiasa na watu waliokuwa karibu na Serikali, baada ya kutofautiana na utawala wa Rais Kagame.
Post a Comment
toa maoni yako hapa pia usisahau kuweka coment