0
Esther Murugi
Mbunge wa Nyeri Mjini Esther Murugi. Picha/JOSEPH KANYI 
Na EVALYNE GITHINJI
MBUNGE wa Nyeri Mjini Bi Esther Murugi, Ijumaa hii alishangaza wanahabari aliposema alilazimisha kufua shiti alizolalia wifi yake aliyekuwa ameenda kujifungua katika hospitali kuu ya Nyeri.
Bi Murugi alisema kisa hicho kilitokea siku mbili kabla ya kisa ambapo mwanamke alipoteza mwanawe aliyedunda sakafuni alipokuwa akijifungua.
“Nilimtembelea wifi yangu katika hospitali hiyo alipokuwa ameenda kujifungua. Hakuweza kujipindua kitandani baada ya kujifungua. Hata shuka zilikuwa hazijaoshwa. Ilinibidi mimi na familia yangu kuziosha shuka hizo,” akasema.
“Sio muuguzi aliyetuhudumia bali ni mwanafunzi wa uuguzi. Baada ya kumuuliza kwa nini jamaa wetu hakuwa ameshughulikiwa, alisema mama akizaa mtoto ni wake,” akaongeza mbunge huyo ambaye zamani alikuwa waziri.
Hata hivyo mkuu wa hospitali hiyo Bw Cyrus Njoroge alimfahamisha Bi Murugi kuwa angejaribu kuyapeleka malilio hayo katika ofisi zao kuu ili kuhakikisha jambo kama hilo limetatuliwa.
Alieleza kuwa baada ya wifi yake kutoka hospitalini, siku tatu hazikuisha kabla ya kisa hicho cha mama kupoteza mtoto kutokea.
Bi Charity Wanjiku mwenye umri wa miaka 27, alimpoteza mwanawe alipokuwa akijifungua mnamo siku ya Januari 15 katika hospitali hiyo ya Nyeri.
Bi Wanjiku alilalamika kuwa mtoto huyo alifariki kufuatia kutoshughulikiwa vyema na wauguzi alipokuwa anajifungua kwani badala ya kushauriwa vyema walimuachilia kujifungua kama amesimama.
Familia ya Bi Wanjiku inangojea ripoti kamili kuhusu tukio hilo kutoka kwa wizara ya afya iliyofanya uchunguzi.
Bi Murugi pia alionya jinsi serikali haina wafanyikazi wa afya wa kutosha haswa kufuatia tangazo la wauguzi kugoma baada ya siku 14, kama hospitali za umma hazitawaajiri wauguzi zaidi.
Alisema kuwa ni jambo la huzuni jinsi wagonjwa wanatatizika kufuatia ukosefu wa wauguzi wa kutosha.
Kulipwa vyema
“Hakuna yule anaweza kuwalaumu wafanyikazi wa afya ambao hutafuta kazi nje ya nchi kwani huko wanalipwa vizuri, serikali yetu inafaa kuwalipa vizuri,” alisema zaidi.
Bi Murugi alisema hayo alipokuwa ameenda kumtembelea mama aliyejifungua katika hospitali hiyo na kupata pacha watatu mfululizo.
“Mimi nilielezwa na kasisi ambaye aliona habari ya mama huyu aliyejifungua watoto watatu lakini hana uwezo wa kifedha na nikaamua kuja kumsaidia,” alisema Bi Murugi.
Mbunge huyo alisema kuwa anafanya kila juhudi kuhakikisha kwamba mama huyo amesaidika kifedha kwa kutafuta wahisani wema ili kumsaidia kuwalea watoto hao.
Bi Naomi Maina, 26, bado amelazwa katika hospitali hiyo, akingojea watoto hao kukomaa kikamilifu ndipo atoke.
Bi Maina alijaliwa watoto hao mnamo siku ya Januari 22 na huku akiwa amejawa na furaha alishukuru kupata msaada kutoka kwa Bi Murugi.

Post a Comment

toa maoni yako hapa pia usisahau kuweka coment

 
Top

SOMA HABARI KEM KEM KUPITIA BLOG YAKO PENDWA YA HISIA ZA MWANANCHI HAPA

X